Mansura ni mwaliko wa safari ya kuelekea katika Hekaya za Wakae, wakaazi wa nchi ya dongo jekundu, iliyopo kusini mwa kisiwa cha Unguja, ambako ulikuwa ukiweza kufika kwa kupanda gari nambari 10.
Ni usanifu wa ulimwengu uliojengeka katika fikra na mawazo yaliyosarifiwa kwa ustadi mkubwa na kumwingiza msomaji katika jahazi la msafara mrefu unaompeleka katika Bahari ya Hindi, yenye mikondo inayopanda na kushuka, na kuakisi maisha ya Wakae. Kwa mchanganyiko wa Kiswahili fasaha na Kikae, mwandishi anafungua milango ya kuifahamu misingi na mitazamo ya kimaisha, mila, utamaduni na itikadi za kusini mwa kisiwa cha Unguja. Hekaya za Wakae zinambeba msomaji kitikiti, kumpandisha na kumshusha, kumpeleka mbele na kumrudisha nyuma katika dahari mbalimbali za maisha zilizoacha chapa katika visiwa vya karafuu. Kwa ustadi mkubwa mwandishi anampaaisha na kumrudisha chini msomaji wake, huku saa yake ikenda mbele na kurudi nyuma, kwa usafiri wa baskeli, gari la punda na gari la matwana, pamoja na vyombo vyengine vinavyoonekana na visivyoonekana. Kama smaku mwandishi anamvuta na kumgandisha msomaji katika tafakuri kubwa inayomkumbanisha na viumbe vya kila aina, vile vyenye maumbo ya kuvutia na vile vyenye maumbo ya kutisha, vile vinavyoishi hewani, na vinavyoishi ardhini na baharini.
Kwa falsafa na mantiki kubwa, mwandishi anajaribu kwa kiwango cha uwezo wake kuweka kumbukumbu za mifumo ya kimaisha, vipaji na makarama ya wakaazi wa sehemu za kusini Unguja, ambazo taratibu zinapotea. Issak yuko hadhir kabisa juu ya athari ghasi za kutoka nje juu ya mifumo ya maisha na ustawi wa jamii ya Wazanzibari.
Mansura ni jitihada za mwandishi katika harakati za kuokoa japo chembe yale muhimu aliyoyajua kwa kuyaishi na kuyasikia, yaliyojenga mustakabali wa maisha yake yeye mwenyewe na jamii yake ya Wakae. Jamii ambayo imetoa mchango mkubwa katika historia ya nchi. Kwa jumla, hisia, njozi, imani za kidini na kidunia, mazingira na mazingara yaliyofafanuliwa katika kitabu hichi yanayowakilisha Wakae, yana taathira na kuakisi pia kwa kiasi kikubwa maisha ya jamii mbali mbali za visiwani na utambulisho wa Zanzibar na Waswahili kwa jumla.
Mohamed A. Saleh
Details
- Publication Date
- Mar 2, 2026
- Language
- Swahili
- ISBN
- 9781291815900
- Category
- Fiction
- Copyright
- All Rights Reserved - Standard Copyright License
- Contributors
- By (author): Issak Esmail Issak
Specifications
- Pages
- 528
- Binding Type
- Paperback Perfect Bound
- Interior Color
- Black & White
- Dimensions
- A5 (5.83 x 8.27 in / 148 x 210 mm)